Ads (728x90)

Inaendeshwa na Blogger.




 
BAADA ya kusota kwa muda mrefu katika ligi daraja la kwanza timu ya soka ya Maji Maji Maarufu kama ‘wanalizombe’ toka mkoani Ruvuma imefanikiwa kurudi ligi kuu baada ya kuifumua Mlale JKT bao  2-1 hivi karibuni katika mtanange wa ligi daraja la kwanza uliofanyika kwenye uwanja wa Maji Maji Songea.

Maji Maji mabingwa wa kombe la Muungano mwaka 1985,1986 pamoja na 1998 imefanikiwa kurudi ligi kuu ya Vodacom toka iliposhuka kwa mara ya mwisho msimu ya mwaka 2010/2011 baada ya kutokea mgogoro kati ya wanachama pamoja na viongozi tatizo likiwa ni wasi wasi wa wanachama kuhusu matumizi ya pesa za timu toka kwa mdhamini wao.

Akizungumza na  Jelamba viwanjani Meneja wa timu hiyo God Mvula alisema baada ya kupata ushindi dhidi ya Mlale JKT mji wa songea na viunga vyake ulizizima kwa furaha na vifijo huku mashabiki wa timu hiyo wakicheza ngoma ya Lizombe ambayo ni maarufu sana mkoani Ruvuma.

“tumepanda ligi kuu kulingana na msimamo wa ligi ulivyo kilichobaki ni kuhakikisha tunafanya vizuri katika mechi yetu ya mwisho dhidi ya Kimondo ili kuwadhiilishia wapenzi wa timu yetu kuwa tulijiandaa vizuri na hatujabahatisha’alisema  Mvula.

Pia Mvula alisema mara nyingi timu ya Maji maji inashuka Daraja kwa tatizo la migogoro kati ya wanachama pamoja  na viongozi suala ambalo  wanalifanyia kazi kwa pamoja ili kuhakikisha timu hiyo inaendeshwa kisasa na kurudisha makali yake ya zamani.

Timu ya maji maji imefikisha pointi 43 na kushika nafasi ya pili nyuma African Sports ambayo imefikisha pointi 45 katika msimamo wa kundi A ambapo kwa sasa kwa mtokeo ya uwanjani timu hizo zimepanda Daraja na hakuna timu ambayo inaweza ikafikisha pointi hizo.
 


Chapisha Maoni