Ads (728x90)

Inaendeshwa na Blogger.






Klabu ya Daraja la Kwanza ya Sonderjyske Fodbold ya nchini Denmark, imemnasa mshambuliaji Emmanuel Okwi na kumpa mkataba wa miaka mitano.

Pamoja na dau la usajili kuonekana ni siri, lakini Okwi atakuwa akilamba mshahara wa dola 10,000 (Sh milioni 20) kwa mwezi.
Kiasi hicho cha mshahara kinamfanya Okwi kuwa mchezaji mwingine aliyeuzwa na Simba anayelipwa fedha nyingi nje ya nchi, baada ya Mbwana Samatta ambaye TP Mazembe ya DR Congo inamlipa dola 10,000 kwa mwezi pia.
Mkurugenzi wa Sonderjyske, Hans Jorgen Haysen, ameiambia SALEHJEMBE, walikuwa wakimfuatilia Okwi kitambo sasa.
“Tulianza kumfuatilia baada ya kusikia taarifa zake, wakati mwingine tuliambiwa na Kocha wa The Cranes (Uganda), Micho kuwa ndiye Ronaldo wa Uganda. Tunafurahi kufikia naye makubaliano naye ya miaka mitano na tayari tumesaini mkataba baada ya kuwa amefuzu vipimo,” alisema.
Kwa mujibu wa bosi huyo wa Sonderjyske, tayari Okwi amepata kibali cha kufanya kazi nchini Denmark na jana alianza mazoezi rasmi.
“Tayari ameanza mazoezi, tulifanya kazi ya kumtambulisha na kumkabidhi jezi aliyokuwa akiitaka ambayo ni namba 25, baada ya hapo amefanya mazoezi na wenzake.
 “Kesho (leo), tutacheza mechi ya kirafiki dhidi ya timu kutoka Ujerumani. Okwi atakuwa kati ya watakaocheza ili kumtambulisha mbele ya mashabiki wa Sonderjyske,” alisema Haysen.
Mshahara wa dola 10,000 unamfanya Okwi kupokea mara tatu ya ule aliokuwa akilipwa Simba wa dola 3,000.
Ligi Kuu ya Denmark inatarajiwa kuanza wiki ijayo na Okwi hatarejea Uganda, badala yake ataungana na wenzake kwa ajili ya mazoezi na baadaye mechi za kirafiki halafu mechi za ligi.
Na Saleh Ally


Chapisha Maoni