Ads (728x90)

Inaendeshwa na Blogger.


 
CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) kinatarajia kushiriki kwenye Mkutano Mkuu wa 78 wa Chama cha Kimataifa cha Waandishi wa Habari za Michezo (AIPS) unaotarajiwa kuanza kesho (Jumatatu) Paris, Ufaransa.
TASWA katika mkutano huo itawakilishwa na Mwenyekiti wa chama, Juma Pinto na Katibu Mkuu, Amir Mhando ambao wanatarajiwa kuondoka Dar es Salaam leo (Jumapili) alasiri kwa ndege ya Emirates wakipitia Dubai.

Mkutano huo wa kawaida wa mwaka ambao utamalizika Machi 4, 2015 utashirikisha viongozi wa zaidi ya vyama vya waandishi wa habari za michezo 150 duniani, utaambatana na mijadala pamoja na semina mbalimbali kuhusiana na uandishi wa habari za michezo.
Pia kutatolewa taarifa kuhusiana na maandalizi ya michezo ya Olimpiki itakayofanyika mwaka 2016 Rio de Jainero, Brazil, ambapo mhusika mkuu atakuwa Mkuu wa Masuala ya Habari wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki (IOC), Anthony Edgar.
Baadhi ya mada zingine katika mkutano huo zitatolewa na wawakilishi kutoka Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Shirikisho la Soka Ulaya (UEFA).Pia kutakuwa na uwasilishaji wa mada kwa vyama mbalimbali vya kimataifa vya michezo.
Pia washiriki watapata mafunzo ya changamoto zinazokabili uandishi wa habari za michezo kutokana na kuenea haraka kwa mitandao ya kijamii.

TASWA inalishukuru Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Kampuni ya Jambo Concepts inayochapisha gazeti la JamboLeo kwa kugharamia tiketi za ujumbe huo.
 TASWA ni mwanachama hai wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Duniani (AIPS) chenye makao yake makuu Lausanne, Uswisi, ndiyo sababu kila mwaka tumekuwa tukishiriki mikutano hiyo.


Chapisha Maoni