Ads (728x90)

Inaendeshwa na Blogger.






Kocha Mkuu wa timu ya taifa ya Tanzania 'Taifa Stars', Mart Nooij leo ametangaza kikosi cha wachezaji 28 watakaoingia kambini katika hoteli ya Tansoma iliyo eneo la Gerezani jijini Dar es salaam, kujiandaa na michuano ya kombe la COSAFA na kuwania kufuzu kwa AFCON na CHAN mwezi Juni mwaka huu.


Akizungumza na waandishi wa habari leo makao makuu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), amesema wachezaji 28 aliowaita, amewaona kwa macho yake wakicheza, na katika wachezaji aliowaita amechanganya wanaochipukia (damu changa) na wenye uzoefu wa michuano ya kimataifa.



Nooij amesema katika orodha hiyo ya wachezaji 28 watakaoripoti kambini jumatatu mchana, watapimwa afya zao na madakatari wa timu ya Taifa, na kisha watakaokuwa fit atachagua wachezaji 20 watakaokwenda kwenye michuano ya COSAFA nchini Afrika kusini.

Aidha Nooij ameongeza wachezaji 8 watakaobakia nchini wanapaswa kuwa tayari wakati wowote wanaweza jumuishwa katika kikosi kutokana na Taifa Stars kukabiliwa na michuano mbalimbali ambayo pia inahitaji kuwa na wigo mpana wa wachezaji.

Wachezaji walioitwa na kocha Nooij ni magolikipa: Deogratius Munish (Yanga), Aishi Manula, Mwadini Ali (Azam), walinzi: Shomari Kapombe, Aggrey Morris, Erasto Nyoni (Azam), Nadir Haroub, Oscar Joshua, Kelvin Yondani (Yanga), Abdi Banda, Hassan Isihaka (Simba), Salim Mbonde (Mtibwa Sugar) na Haji Mwinyi (KMKM).

Wengine ni viungo: Amri Kiemba, Salum Abubakar, Frank Domayo (Azam), Said Juma 'Makapu', Salum Telela, Hassan Dilunga (Yanga), Said Ndemla (Simba), Haroun Chanongo (Stand United) na Mwinyi Kazimoto (Al Markhiya).

Washambuliaji ni Ibrahim Ajibu (Simba), Mrisho Ngasa, Simon Msuva (Yanga), John Bocco, Kelvin Friday (Azam) na Juma Luizio (Zesco United).

Taifa Stars inatarajiwa kuondoka nchini siku ya jumatano, Mei 13 saa 1 jioni kwa shirika la ndege la Fastjet kuelekea nchini Afrika Kusini katika mji wa Rusterburg - North West Province ambapo ndipo michuano ya COSAFA CUP itafanyika kuanzia Mei 17 mpaka Mei 31 mwaka huu.

Mchezo wa kwanza wa Taifa Stars iliyopo katika kundi B katika michuano ya COSAFA, itacheza dhidi ya Swaziland Mei 18, Mei 20 (Madagascar Vs Tanzania) na Mei 22 ( Tanzania vs Lesotho), mshindi wa kundi B atacheza robo fainali dhidi ya timu ya Taifa kutoka Ghana.

Mara baada ya kumalizika kwa michuano hiyo, Taifa Stars itarejea nchini kujiandaa na mchezo wa kuwania kufuzu kwa AFCON 2017, dhidi ya Misri utakaopigwa Juni 13 nchini Misri, kisha kurejea nchini kucheza na Uganda Juni 21 kuwania kufuzu kwa fainali za wachezaji wa ndani CHAN.


Mart Nooij amesema ataitumia michuano ya COSAFA kama sehemu ya maandalizi ya michezo ya kuwania kufuzu kwa AFCON na CHAN.

IMETOLEWA NA MSEMAJI WA TFF, BARAKA KIZUGUTO


Chapisha Maoni