Ads (728x90)

Inaendeshwa na Blogger.



Itakumbukwa Agosti 26,1979 Taifa Stars ilikuwa ikihitaji sare ya aina yoyote dhidi ya Zambia ili ifuzu kushiriki Fainali za Mataifa ya Afrika kwa mara ya kwanza tangu ilipoanza kushiriki mwaka 1968.
Taifa Stars ilikuwa ikicheza mechi hiyo ya marudiano dhidi ya Zambia kuwania kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika za mwaka 1980 zilizofanyika Lagos, Nigeria.
Katika mechi ya kwanza iliyozikutanisha timu hizo, Taifa Stars iliilaza Zambia bao 1-0 ambalo lilifungwa na kiungo, Mohammed Rishard Adolph.
Mechi ya marudiano ilichezwa mjini Ndola, nje kidogo ya jiji la Lusaka na timu ya Zambia ndiyo ilikuwa ya kwanza kupata bao mwanzoni mwa mchezo, lakini Taifa Stars ilisawazisha bao hilo mfungaji akiwa Peter Tino.
Bao hilo la Tino lilinyamazisha umati wa mashabiki wa Zambia waliokuwapo uwanjani kwani liliiwezesha Taifa Stars kufuzu kushiriki Fainali za Mataifa ya Afrika 1980.
Fainali za Lagos
Baada ya kufuzu kushiriki Fainali za Mataifa ya Afrika 1980, katika fainali hizo, Taifa Stars ilichapwa mabao 3-1 na wenyeji Nigeria katika mechi ya ufunguzi, ilitoka sare ya mabao 2-2 na Ivory Coast kabla ya kuchapwa mabao 2-1 na Misri na kutolewa hatua ya makundi.
Kwa miaka 35 sasa, Taifa Stars imekuwa ikisaka nafasi kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika, lakini imeshindwa kuwika.
Fainali za CHAN
Mwaka 2009, Taifa Stars ikiwa chini ya kocha Marcio Maximo kutoka Brazil ilifuzu kushiriki Fainali za Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za ndani ya Afrika (CHAN) baada ya kuichapa Kenya 2-1 na katika mechi ya marudiano iliichapa tena 1-0. Mechi iliyofuata Taifa Stars ilicheza dhidi ya Uganda na kushinda 2-0 na ziliporudiana zilitoka sare 1-1. Mechi ya mwisho Stars iliichapa Sudan 3-1 na ziliporudiana iliibuka na ushindi wa 2-1 na hivyo kufuzu fainali za CHAN.
Hata hivyo, katika fainali hizo za CHAN, Taifa Stars ilifungwa na Senegal 1-0, ikaishinda Ivory Coast 1-0 na ilitoka sare ya 1-1 na Zambia hivyo kutolewa katika hatua ya makundi.
Makocha wa Taifa Stars
(Kocha Marcio Maximo, 2006-2010)
Taifa Stars imekuwa ikinolewa na makocha mbalimbali wa kigeni na wazawa. Mwaka 2006 ilinolewa na kocha Marcio Maximo kutoka Brazil ambaye aliiwezesha Stars kushiriki CHAN 2009.
Kingine alichofanikiwa kocha huyu ni kurudisha ari, moyo na uzalendo kwa wachezaji. Pia Watanzania nao walirudisha moyo wa kuipenda Taifa Stars, walinunua fulana za kuiunga mkono, walifurika uwanjani kuishangilia, tulifungwa, lakini tuliridhika na msingi wa soka ulianza kujengeka chini ya Maximo.
Kocha Marcio Maximo aliiongoza Taifa Stars kuanzia 2006 mpaka 2010 na katika kipindi hicho, Taifa Stars ilicheza mechi 43, kati ya hizo Taifa Stars ilishinda mechi 16, sare 15 na ilifungwa mechi 12.
Pia Maximo alifanya mapinduzi ya aina yake baada ya kuipandisha Tanzania kwenye viwango vya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), kutoka nafasi ya 167 mpaka nafasi ya 108.
(Kocha Jan Poulsen, 2010-2012)
Kati ya mwaka 2010 mpaka 2012, Taifa Stars ikawa inanolewa na kocha Jan Poulsen raia wa Denmark. Kocha huyu alipokuja alikuta Watanzania wamehamasika kuipenda timu yao ya taifa na yeye akaona lipo tatizo ambalo Watanzania wanalifungia macho, tatizo la kuendeleza mchezo wa soka nchini.
Kocha Jan Poulsen akasema,”Watanzania ndiyo wenye jukumu la kuendeleza mchezo wa soka nchini hivyo wanatakiwa kutafuta mfumo thabiti utakaosaidia kufanikisha suala hilo na kuacha mtazamo wa kuangalia timu ya Taifa tu.”
Poulsen alisema anafahamu suala hilo ni gumu kutokana na ukubwa wa nchi, kwani rasilimali za kiuchumi zilizopo zinashindwa kusaidia mchezo wa soka, lakini alisema tunavyozidi kuchelewa kuusaidia mchezo wa soka ndiyo tunavyozidi kurudi nyuma katika mchezo huo.
Kocha Poulsen alisema wachezaji wa Kitanzania anaowachagua Taifa Stars na wanaoendelea kuchaguliwa wanatokana na mfumo ambao Watanzania wameutengeneza ambao haujali soka la vijana.
Poulsen alisema wachezaji wa Tanzania wanakosa kufundishwa mambo mengi katika ngazi za chini kwa sababu anaona mambo mengi aliyokuwa anawafundisha wachezaji kwenye timu ya taifa walitakiwa wafundishwe wakiwa watoto au vijana.
Katika kipindi hiki ndiyo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) likamleta kocha Kim Poulsen kutoka Denmark, ambaye akawa anazinoa timu za taifa za vijana chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) na miaka 20 (Ngorongoro Heroes).
Jan Poulsen alikuwa na mipango mizuri, lakini ilionekana kushindikana kutokana na uharaka wa Watanzania.
Ni kweli Stars ilishuka kiwango ukilinganisha na kipindi cha Maximo, lakini Jan alikuwa na mipango ya muda mrefu.
Jan alitaka Tanzania iwekeze muda na fedha kuandaa timu za vijana, miundo mbinu ya soka, kuandaa makocha wenye ueledi wa juu na kuwa na viongozi sahihi katika nafasi sahihi.
Wakati wa kocha Jan Poulsen, Taifa Stars ilicheza mechi 22, kati ya mechi hizo, Taifa Stars ilishinda mechi 5, ikatoka sare 7 na ilifungwa mechi 10. Pia aliiongoza Kilimanjaro Stars ya Tanzania Bara kutwaa Kombe la Chalenji kwa mara ya kwanza baada ya miaka 16, alipoifunga Ivory Coast kwenye fainali iliyofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
(Kim Poulsen, 2012-2014)
Kocha Kim Poulsen alikuwa akivinoa vikosi vya timu za taifa za vijana na alipandishwa na kupewa jukumu la kuinoa Taifa Stars baada ya TFF kumtimua kocha Jan Poulsen.
Alipokuwa anavinoa vikosi vya timu za taifa za vijana aliweza kuwaibua nyota wengi kama Frank Domayo, Simon Msuva, Ramadhan Singano, Edward Christopher, Idrissa Rashid ‘Baba Ubaya’, Hassan Kessy, Atupele Green, Jerome Reuben Lembele, Frank Sekule, Hassan Dilunga na wengine wengi, ambao baadaye wengine aliwapandisha kuichezea Taifa Stars.
Kocha Kim Poulsen alikubalika kwa wadau na wachezaji, Kim alikuwa anawajua wachezaji wa Kitanzania na alikuwa anatafuta mafanikio yake na Taifa Stars. Kwa wale waliokuwa wanafuatilia mpira uliokuwa ukichezwa na Serengeti na Ngorongoro walikuwa wanafahamu ni kocha mwenye uwezo gani. Aliibadilisha pia Taifa Stars ikaanza kucheza mpira tuliokuwa tunauota, baada ya miaka miwili kupita ya mkataba wake waliokuwa viongozi wa TFF chini ya rais, Leodeger Tenga wakampa mkataba mwingine.
Baada ya mabadiliko ya kiuongozi ndani ya TFF kufuatia Tenga kumaliza kipindi cha pili cha uongozi, aliyekuja kuchukua nafasi ya Tenga baada ya uchaguzi alikuwa Jamal Malinzi. Rais huyu mpya wa TFF alifanya mabadiliko na kumfuta ajira ya kocha Kim Poulsen na ajira hiyo kumpa kocha Mart Nooij raia wa Uholanzi ili aiwezeshe Taifa Stars kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika 2015 jambo ambalo lilishindikana kwani Nooij alishindwa.
Katika kipindi Kim Poulsen alichoinoa Taifa Stars ilicheza mechi 15, kati ya hizo Taifa Stars ilishinda mechi 5, ilitoka sare 4 na ilifungwa mechi 6.
(Kocha Mart Nooij, 2014-2015 )
Kocha Mart Nooij alikuja wakati mbaya kweli kweli, wakati tunaohitaji matokeo, wakati tunaohitaji kushinda, wakati tuliokuwa tunahitaji kufuzu kushiriki Fainali za Afrika 2015, hata hivyo alishindwa kuiwezesha Taifa Stars kufuzu.
Baada ya hapo TFF ilimwambia Mart Nooij kibarua chake kitasitishwa akishindwa kuiwezesha timu hiyo kufuzu mashindano Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za ndani (CHAN 2016), tayari kocha Nooij ametimuliwa jana baada ya Taifa Stars kuchapwa 3-0 na Uganda katika mechi ya kwanza ya CHAN. Pia benchi la ufundi la Taifa Stars limevunjwa kuanzia Juni 21, 2015.
Tangu Mart Nooij aichukue Taifa Stars, tayari timu hiyo imecheza mechi 18 na kati ya hizo imeshinda 3, imetoka sare 6 na imefungwa 9.
Mitazamo mbalimbali
Mart Nooij anasema,”Mafanikio ya soka yanahitaji kucheza kitimu ‘Team Work’, kama utakuwa na mabeki wazuri halafu huna washambuliaji hilo ni tatizo, kama klabu itakuwa na wachezaji wazawa wazuri kwenye kikosi cha kwanza hakuna shaka timu ya taifa itakuwa nzuri pia.
“Tatizo jingine baadhi ya wachezaji wanapokuwa timu ya taifa hawajitumi kama wanavyokuwa kwenye klabu zao, wanashindwa kung’amua kuwa mazoezi ya timu ya taifa ni ya muda mfupi hivyo wajitume, lakini wengine wanakuwa wavivu, hilo ni tatizo katika kufanya vizuri,” anasema Nooij.
Kocha msaidizi wa Yanga, Boniface Mkwasa anasema, “Taifa Stars inapata kila inachohitaji na mdhamini anajitoa kwa hali na mali kuhakikisha hakuna kinachokosekana kwa wachezaji na benchi zima la ufundi, Taifa Stars inapofanya vibaya ni lazima TFF itafute njia za haraka kutafuta ufumbuzi wa tatizo,” alisema Mkwasa.
Naye kocha wa Yanga, Hans Pluijm anasema, “Katika mechi dhidi ya Misri, makosa binafsi pamoja na maandalizi ya chini kwa timu hiyo ndiyo yameigharimu, wachezaji walionekana kama hawajaandaliwa vizuri kisaikolojia kabla ya pambano lile jambo liliowafanya waonekane hawajiamini katika muda mwingi wa mchezo.”
Kwa upande wake Mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Aden Rage amemtaka Rais wa TFF, Jamal Malinzi kumtimua kazi kocha wa Stars, Mart Nooij kwa kuwa ameshindwa kuivusha Tanzania katika medani ya soka.
“Kocha wa Taifa Stars ameshindwa kazi, ameonyesha hawezi, sasa Malinzi ampe chake aondoke, wanamng’ang’ania wa nini?, kila siku hatuna raha kwa nini? Hata Ulaya, makocha wanatimuliwa kwa kushindwa kufanya kile kinachokusudiwa,” alisema Rage.
Nyota wa zamani wa Taifa Stars, Sunday Manara anasema,”Nchi nyingine wachezaji wa zamani wanakuwa karibu na benchi la ufundi, wanashahuri, lakini Tanzania kitu hiko hakipo, mchezaji wa zamani hupewi nafasi.
“Tena ukionekana unachangia unaanza kubezwa, hili ni tatizo, ndiyo sababu kila siku tunazidi kuporomoka badala ya kupanda, mifumo ya soka letu inapotea,” anasema Manara.
Mkuu wa Idara ya Michezo kwenye Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine, Padri Leone Maziku anasema,”Kocha Marcio Maximo anabakia kuwa pekee ambaye alionyesha mwanga wa kulitoa soka la Tanzania kutoka hatua moja kwenda nyingine, kocha huyu aliweka msingi imara wa timu ya Taifa kwa kuwaandaa wachezaji wengi wenye umri mdogo ambao baadaye waligeuka kuwa lulu Taifa Stars na kwenye klabu zao.
“Maximo alitambua udhaifu wa mfumo wetu wa soka na aliamua kuutafutia mwarobaini kwa kukusanya na kuwapa nafasi wachezaji wengi chipukizi kwenye kikosi cha timu ya Taifa, jambo lililowafanya vijana hao kukomaa mapema kiushindani, pia aliwahamasisha Watanzania waipende timu yao ya Taifa jambo ambalo wenzake waliofuatia wameshindwa kulifanya,” alisema Maziku.
Kocha wa zamani wa Kurugenzi FC ya Iringa, Zulfikar Mahadi anasema kuwa katika makocha wanne ambao wameinoa Stars ndani ya kipindi cha miaka 10 iliyopita, Marcio Maximo bado rekodi zake hazijafikiwa na wote waliomtangulia.
Mahadi anasema ingawa Maximo alilikuta soka hapa nchini likiwa limedoda, alijitahidi kuliinua na kuwafanya wengi warudishe mapenzi yao kwa mchezo huo hapa nchini.
“Kwenye soka tunapima mafanikio ya timu kwa kuangalia kiwango cha uwanjani na matokeo yanayopatikana, Maximo alijitahidi kuifanya timu yetu ipate matokeo mazuri,” anasema Mahadi.
Kocha Msaidizi wa Stand United, Athuman Bilali yeye amewataja Maximo na Kim Poulsen kuwa walikuwa chaguo sahihi kwa timu ya Taifa.
Bilali anasema kuwa ingawa kuna tatizo kwenye mfumo wa soka letu hali inayowapa wakati mgumu makocha wanaopata fursa ya kuinoa timu ya Taifa, lakini Kim na Maximo walifanikiwa kwa kiasi fulani kuibadilisha Stars.
Bilali anasema kuwa makocha hao waliifanya Taifa Stars iwe na sura ya kitaifa na ilileta ushindani kwa timu ambazo ilikutana nazo.
Hata hivyo, wapo wadau wengine wengi ambao wanaona tatizo la Taifa Stars siyo makocha bali ni wachezaji wa Tanzania kwani wanakosa mambo mengi ya msingi kama kukokota mpira, kupokea mpira, kutuliza kwa usahihi, kupiga pasi sahihi, kupiga pasi za kichwa, kuulinda mpira, kupiga mashuti sahihi, kunyang’anya mpira, kurusha mpira, upigaji wa faulo zenye ufundi, kuokoa mpira, upigaji wa kona, mbinu za ushambuliaji, ulinzi, ushambuliaji, mfumo wa ufungaji mabao, ukipa mzuri, umakini na matumizi ya juu ya akili uwanjani.
Kutokana na wadau wengine kuonyesha tatizo ni makocha na wengine wakidai ni wachezaji ndipo swali linakuja, je, tatizo la Taifa Stars ni makocha au wachezaji?.



Chapisha Maoni