Ads (728x90)

Inaendeshwa na Blogger.




Na Alex Mapunda,Iringa

JINA la Saidi  Abdallah Chitalula sio geni kwa wadau wa soka Mkoani Iringa,kwa vile ameitumikia Lipuli katika nyakati tofauti kama mchezaji na Meneja wa timu hiyo.

Chitalula mzaliwa wa Morogoro alianza kusakata kandanda akiwa shule ya Msingi Mbuyuni, mwaka 1980 na baadae katika sekondari ya Jabalhilahh, lakini alikatisha masomo kidato cha tatu baada ya baba yake kufariki na familia ikakosa fedha ya kumpeleka shule.

Mwaka 1990 alijiunga na chuo cha ufundi Morogoro(genaral course In Engeenering[  hapo ndipo alipopata bahati ya kujiunga na timu ya daraja la nne ya Fruits Fc timu ya wafanyabiashara wa matunda.

Baada ya nyota yake kung'aa akasajiliwa na timu ya Mnadani Fc katika ligi daraja la tatu ambayo aliitumikia toka mwaka 1993 hadi 1995, mwaka ambao alisajiliwa na Geto Afrika ya ligi daraja la tatu.

1996 hadi 1998 alicheza kwa mafanikio makubwa akiwa na timu ya Magereza ya Iringa timu ambayo waliipandisha hadi ligi daraja la pili hapo ndipo akanyakuliwa na Polisi Morogoro lakini baadae aliachana nayo baada ya kuhaidiwa kazi ya Jeshi lakini akatoswa dakika za mwisho.

Mwaka 2000 alisajiliwa na Chelsea ya bongo(Moro United) na akaichezea muda mfupi baadae akajiunga na Lipuli ya Iringa 2001.

Kufuatia Lipuli kushuka daraja mwaka 2001 akatimukia zanzibar katika timu Hardrock Fc ya Pemba lakini kutokana na Maslai Mabovu,pia rafiki zake walimwambia akicheza Zanzibar ni raisi kwenda uarabuni na  iliposhindikana, akaamua kustaafu kucheza mpira.

Kwa kipindi chote ambacho Chitalula amekuwa Mchezaji na meneja wa Lipuli amekumbana na mambo mengi,yeye mwenyewe anafafanua.
Sababu za kutokucheza Simba na Yanga.

"Kila nikifikia nakosa jibu kwa kuwa sababu iliyoninyima ulaji yanga ndio ile ile iliyotokea kwa Simba"

"Mwaka 1994 wakati nikiwa moto,kocha wa Simba Athumani Juma alinichukua kwenda kufanya majaribio na nilifanikiwa kucheza mechi mbili kubwa lakini baadae dili la kusajiliwa liliota mbawa baada ya kutokea mgogoro ndani ya Simba na kocha aliyetaka kunisajili akafukuzwa kazi"

"Pia 2001 yanga ikiwa chini ya kocha Charles Mkwasa pamoja na Minziro walitaka kunichukua lakini nao wakafutwa kazi muda mfupi kabla ya kunisajili".

Ushirikina

"Upo ni mkubwa sana licha ya kwamba hauna msaada,mimi nilipokuwa timu ya Magereza ya Iringa tulienda kucheza katika kituo cha kigoma kupigania kupanda ligi daraja la pili tukatafuta mtalam wa kutufanyia dawa baada ya wenyeji kutuambia kuwa ni ngumu kucheza mpira Kigoma bila kamati ya ufundi nje ya uwanja"

"Nakumbuka alikuja mzee mmoja ambaye mwili wake uliisha kwa ukoma alitufanyia dawa usiku kucha, hali ambayo ilipelekea wachezaji kuchoka kwa usingizi,wakati wa mechi tulifungwa bao 4-1 na Toto Africa"

"Mechi zilizofuata tukacheza bila dawa,tukashinda zote na tukachukua ubingwa,pia Tanga tulivunja Nazi tukafungwa bao 5-2 dhidi ya TPC Moshi".
Dhuluma.
“timu nyingi za Tanzania toka miaka ya nyuma zinawadhulumu sana wachezaji na mara nyingi wachezaji wakidai haki zao wanaingizwa kwenye kundi la utomvu wa nidhamu,nilipokuwa timu ya Moro united kulikuwa na ubaguzi wa wazi wazi kwa wachezaji”
“Kiongozi wa moro united Mbarack maarufu kwa jina la Mbale baadhi ya wachezaji aliwalipa posho kubwa kuliko wengine kuna kipindi nilienda kuchukua fedha akaniambia hazipo wakati mchezaji mwenzangu nilipishana nae mlangoni akitoka kuchukua pesa”

Kushuka daraja kwa Lipuli 2001

"Sababu za Lipuli Kushuka daraja ilikuwa ni mgogoro kati ya wanachama na viongozi,pia uongozi mbovu hali ambayo ilipelekea timu kukumbwa na ukata mkubwa sana"

"Nakumbuka wachezaji tulilazimika kwenda kufanya kibarua ili kupata chakula mimi namshukuru mungu mama yangu ni mzaliwa wa Iringa hivyo baada ya mazoezi nilikimbilia kwa bibi kupata chakula"

"Hadi mwisho wa siku timu ikashuka daraja,baada ya kushuka timu haikuwa na pesa ya kuwapa wachezaji nakumbuka rafiki yangu..(jina linaifadhiwa) aliiba magodoro mawili katika gesti ambayo tulipangiwa na timu ili kupata nauli  na wachezaji wengi walikwama kuondoka kwa wiki kadhaa"

Siri ya Lipuli
“hadi leo hii mimi bado sijapata jibu kati ya mwenyekiti wa Lipuli,Abuu Changawa Majeck pamoja na Katibu wille Chikweo ni nani anadhamira ya kweli ya kupandisha Lipuli ligi kuu”
“kuna kipindi wanakuwa kitu kimoja na kuna wakati kila mmoja anamtuhumu mwenzake anauza mechi za timu”
“mimi nilikuwa Meneja wa Lipuli Msimu uliopita ambao Maji Maji na African Sports walipanda ligi kuu, wakati najiunga na timu wachezaji walikuwa katika vita na mwenyekiti wa Lipuli kwa kesi za kuuza mechi na vyombo vingi vya habari viliripoti kuhusu Majecki”
“Mimi nikasaidiana nao kujenga timu lakini baadae nikachukiwa na katibu wa timu Wille chikweo kwa kuwa nilkuwa na msimamo chanya na timu hasa matumizi mazuri ya fedha za timu kwa wachezaji,katibu mara nyingi alikuwa na mambo yake binafsi kuhusu fedha za timu baadae wakaniundia zengwe la kuniondoa hadi wachezaji wakakataa kusafiri bila mimi, lakini baada ya msimu kuisha wakaniondoa na matokeo yake msimu huu timu inapigania kushuka daraja “.
Ujenzi wa Lipuli.
“Lazima ufanyike uchagunzi na wapatikane viongozi wapya, viongozi waliopo mfano mwenyekiti na katibu kama watarudi wasiwe viongozi wakuu wawe wa kawaida kama wajumbe tu,ila wapo wenye machungu na timu kama vile Ronjino malambo katibu msaidizi [anaweza]”
“Kwa viongozi waliopo sasa hivi hata kama waandishi wa habari watanikutanisha nao nitaeleza ukweli kwa kumchambua mmoja baada ya mwingine,nayajua maovu yao yote na mazuri yao”
Soka la Tanzania
“viongozi ni wabovu toka ngazi ya wilaya,ili tusonge mbele tuwaondoe na tuanzie na soka la vijana”.
Tukio kali.
“tukiwa na timu ya magereza kambini Tanga,kuna mchezaji mwezangu Chuma Kisigalile  kwa sasa yupo Dar, alipata maneno ya uzushi toka kwa wachezaji wezake kuwa mimi nilimkandia kwa viongozi na kocha ili asipangwe kwa sababu ambazo hazikufahamika”
“Basi Kisigalile alipandwa na hasira kisha akachukua ndoo ya chuma yenye maji na kuingia katika chuma ambacho tulilala na kuita jina langu kwa nguvu na tulikuwa wachezaji wengi na wengine walikuwa wakicheza drafti, mimi baada ya kuitika alirusha ile ndoo kwa nguvu nikakwepa, spidi ya ile ndoo ilikuwa kali hadi ilitoboa ukuta”
“baada ya pale viongozi wakatuita na tukamaliza tofauti zetu hadi leo mimi na Kisigalile ni marafiki wakubwa.
Tofauti ya soka la zamani na sasa.
soka la zamani wachezaji walikuwa wakijituma sana na ilikuwa ngumu sana kuchukua hongo,soka la sasa hivi wachezaji wanaangalia sana fedha badala ya kujituma”.
Mchezaji Mkali
“Namkubari sana Donald Ngoma wa yanga anajituma sana”

Maisha baada ya soka.
“Nina umri wa miaka 43 nina mke na watoto wane[nilifunga ndoa mwaka 2013] kwa sasa bado najiusisha na soka kama mshauri na nafanya biashara ndogo ndogo,anahitimisha Saidi Chitalula, Mchezaji  ambaye amecheza madaraja yote ya ligi za hapa Tanzania.


Chapisha Maoni