Ads (728x90)

Inaendeshwa na Blogger.


Na Ameir Khalid, ZANZIBAR
SIKU moja baada ya Mahakama Kuu
ya Zanzibar kuwaamuru viongozi wa
juu wa Chama cha Soka (ZFA)
kuondoka madarakani, kamati ya
muda kwa ajili ya kusimamia shughuli
za chama hicho imeundwa.
Juzi, Jaji wa Mahakama Kuu ya
Zanzibar Mkusa Isaac Sepetu, wakati
akisikiliza kesi inayowakabili viongozi
hao, Rais wa ZFA Ravia Idarous,
Makamu wake ofisi ya Pemba Ali
Mohammed pamoja na Katibu Mkuu
Kassim Haji Salum, alisema kwa
mujibu wa katiba ya ZFA muda wao
wa kukaa madarakani umemalizika
hivyo wakae pembeni.
Rais wa aliyeondolewa madarakani
ZFA na Mahakama, Ravia Idarous
kulia akiwa na rais wa zamani wa
ZFA, Ali Ferej Tamim na Kocha
Shaaban Ramadhani kushoto
Jaji Sepetu pia alitoa agizo la
kuundwa kamati ya muda ya uongozi
wa chama hicho ambacho mbali na
kesi ya ubadhirifu wa fedha,
inakabiliwa na kesi mbili za kukiuka
katiba na kanuni za mashindano,
zilizofunguliwa dhidi yake na klabu za
Chuoni SC na Aluta.
Kufuatia amri hiyo ya mahakama,
Umoja wa Klabu za Soka Zanzibar
umetaja kamati ya watu saba ambayo
itakuwa na jukumu la kuweka mambo
sawa ili shughuli za mpira wa miguu
ziendelee, pamoja na kujipanga kwa
ajili ya uchaguzi mkuu wa chama
hicho kupata viongozi wapya.
Akizungumza na waandishi wa habari
jana katika ukumbi wa uwanja wa
Amaan, Katibu wa umoja huo Ali Ussi
Jongo, aliwataja walioteuliwa kuunda
kamati hiyo kuwa ni Hussein Ali
Ahmada anayekuwa Mwenyekiti
ambapo Makamu wake atakuwa Omar
Ahmed Awadh.
Aidha, Hashim Salum Hashim
anakuwa Katibu Mkuu akisaidiwa na
Khamis Hamad, wakati Masoud Attai
Masoud, Salum Hamdun na Ali Ussi
Jongo wanakuwa wajumbe wa kamati
hiyo.
Jongo alisema miongoni mwa
majukumu makubwa ya kamati hiyo ni
kuzungumza na uongozi wa klabu za
Chuoni SC na Aluta, kuziomba
ziondoshe kesi walizoifungulia ZFA ili
mpira uchezwe na ligi zianze.
Aidha, alisema kazi nyengine ni
kuandaa utaratibu wa kufanya
uchaguzi mkuu wa chama hicho
ambacho kwa muda sasa shughuli
zake zimekwama kutokana na
kuelemewa na mzigo wa kesi
mahakamani.
Akizungumza na gazeti hili baada ya
kuteuliwa kwake, Mwenyekiti wa
kamati hiyo Hussein Ali Ahmada
(pichani) ambaye pia ni Katibu wa
kituo cha kukuza vipaji cha Oranje
(OFA), alisema kazi waliyopewa ni
ngumu lakini anaamini wakipata
ushirikiano wataifanya kwa ufanisi
mkubwa.
"Kwa kuwa nia yetu sote ni kuona
soka linachezwa na kuendelea, na pia
mimi nilikuwemo kwenye kamati ya
usuluhishi kumaliza mzozo ndani ya
ZFA, bila shaka kwa pamoja tutaweza
kurejesha hali kuwa ya kawaida,"
alifafanua.
Taarifa zaidi zilizopatikana na gazeti
hili, zimefahamisha kuwa, ifikapo
Jumamosi, mambo yote
yanayokwamisha shughuli za ZFA
yatakuwa yamemalizwa na kubaki
kuwa historia.
Source bin zubeiry



Chapisha Maoni